DAR ES SALAAM — Tanzania imetaja maeneo manne ya kipaumbele ya kimkakati huku nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (Southern African Development Community – SADC) zikianza awamu ya utekelezaji kamili wa programu ya kikanda ya ushirikiano wa teknolojia ya satelaiti, kutoka hatua ya kushirikiana rasilimali kwenda matumizi ya moja kwa moja ya mifumo ya anga.
Akifungua Kongamano la Satelaiti ya Pamoja ya SADC 2026 jijini Dar es Salaam, Waziri wa Mawasiliano, Habari na Teknolojia ya Habari, Angellah Kairuki, alisema hatua hiyo inaashiria mabadiliko muhimu kuelekea mifumo ya vitendo inayoweza kubadilisha mustakabali wa teknolojia na maendeleo ya kiuchumi ya ukanda.
Kwa mujibu wa waziri, maeneo manne yaliyopewa kipaumbele ni: kilimo na usalama wa chakula, madini na usimamizi wa rasilimali asilia, tabianchi na kukabiliana na majanga, amani na usalama.
Alieleza kuwa teknolojia ya satelaiti inaweza kutumika katika ufuatiliaji wa mazao ili kuimarisha usalama wa chakula, ramani za kijiografia kuboresha usimamizi wa mazingira katika shughuli za madini, mifumo ya uangalizi wa dunia (earth observation) kufuatilia rasilimali za maji na hali mbaya ya hewa, pamoja na zana za anga kusaidia ufuatiliaji wa miji na uratibu wa masuala ya usalama.
“Ni lazima kupanua wigo wetu na kuelekeza teknolojia hizi katika sekta zinazogusa moja kwa moja uchumi wetu,” alisema.
Kongamano hilo, lililofanyika chini ya kaulimbiu “Origins Orbital Frontiers”, linakuja wakati ambao maofisa wa kikanda wanautaja kuwa wa mabadiliko makubwa kwa SADC. Mpango wa satelaiti unaendana na Dira ya Maendeleo ya SADC 2050, inayolenga kuigeuza Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara kutoka mtumiaji wa huduma za anga kwenda mshiriki hai katika uchumi wa kimataifa wa anga.
“Hili si suala la teknolojia pekee,” alisema Kairuki. “Ni suala la uhuru wa kitaifa, ustahimilivu wa kiuchumi na maendeleo jumuishi.”
Tanzania ilisisitiza dhamira yake ya kuimarisha muunganiko wa kidijitali wa kikanda, ikieleza kuwa Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano ya TEHAMA, pamoja na vituo vitano vya nyaya za chini ya bahari (submarine cable landings), umeongeza mawasiliano na nchi jirani za SADC ikiwemo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Malawi, Msumbiji na Zambia.
Kwa mujibu wa waziri, Tanzania pia imeongeza mifumo miwili ya ziada ya usalama inayotumia satelaiti ili kuimarisha uimara wa mitandao ya mawasiliano. Hatua hiyo imeongeza viwango vya mawasiliano kufikia asilimia 98.6 kwa 2G, asilimia 93.4 kwa 3G, asilimia 94.2 kwa 4G na asilimia 30.1 kwa 5G hadi Desemba 2025.
Hata hivyo, alibainisha kuwa miundombinu ya ardhini pekee haiwezi kufikia maeneo ya mbali au kutoa ufuatiliaji mpana wa mazingira, jambo linaloipa teknolojia ya anga umuhimu wa kimkakati.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi na Afisa Mwandamizi wa Programu za TEHAMA wa SADC, George Ah-Thew, alisema mradi wa satelaiti ni miongoni mwa miradi 11 ya kimkakati chini ya Mpango wa Kikanda wa Maendeleo wa SADC.
Alisisitiza kuwa mtandao wa kasi unaotumia satelaiti unaweza kuunganisha shule, vituo vya afya na vituo vya jamii katika ukanda mzima. Hata hivyo, alionya kuwa muda ni jambo nyeti, akisema baada ya miaka sita ya kujenga rasilimali watu wa kitaalamu, nchi wanachama zina dirisha la miaka minane — kwa msaada wa Ofisi ya Usimamizi wa Mradi wa Satelaiti ya Angola — kuufikisha mradi katika utekelezaji kamili.
“Tusipofanya sasa, tunaweza kupoteza fursa hii,” alisema.
Mbali na juhudi za kikanda, Tanzania inaendelea kukuza ajenda yake ya kitaifa ya anga kupitia mpango wa CubeSat KiboCube, unaotekelezwa kwa ushirikiano na United Nations Office for Outer Space Affairs (UNOOSA) na Japan Aerospace Exploration Agency (JAXA), kwa lengo la kujenga uwezo wa ndani kabla ya misheni za kikanda zijazo.
Maofisa walisema matumizi ya satelaiti yanatarajiwa kusaidia upangaji wa kilimo, mifumo ya tahadhari za mapema za majanga, uchimbaji endelevu wa rasilimali na uratibu wa misaada ya kibinadamu katika ukanda wa SADC.









