DAR ES SALAAM — Tanzania imesema imevutia upya maslahi ya wawekezaji wa kimataifa katika sekta ya madini kufuatia ushiriki wake katika Mkutano wa Kimataifa wa Mining Indaba, huku serikali ikiendelea kusukuma mkakati wa kuondoka kwenye usafirishaji wa madini ghafi na kuelekea uchakataji na uongezaji thamani ndani ya nchi.
Mkutano huo, uliofanyika kuanzia Februari 8 hadi 12 mjini Cape Town, Afrika Kusini, uliwakutanisha serikali, kampuni za madini, taasisi za kifedha na wadau wa maendeleo kujadili mwelekeo wa mitiririko ya uwekezaji, viwango vya uendelevu na nafasi ya madini muhimu katika mabadiliko ya nishati duniani.
Katika taarifa yake, Wizara ya Madini ilisema wadau kadhaa wa kimataifa wameonyesha utayari wa kuanza taratibu za uwekezaji nchini Tanzania, hususan katika sekta za uchakataji wa madini (downstream industries), badala ya kusafirisha madini yasiyochakatwa.
“Ushiriki wa Tanzania katika Mining Indaba umefungua fursa mpya za uwekezaji kufuatia mazungumzo ya ngazi ya juu kati ya ujumbe wa Tanzania na wawekezaji wakuu wa kimataifa,” ilisema wizara hiyo. “Wawekezaji kadhaa wa kimataifa wameonyesha wazi nia ya kuanzisha miradi ya uwekezaji katika sekta ya madini nchini.”
Dhahabu kama nguzo, juhudi za kupanua wigo wa madini
Sekta ya madini ni miongoni mwa vyanzo vikuu vya fedha za kigeni nchini Tanzania, ikichangia takribani asilimia 9 hadi 10 ya Pato la Taifa (GDP) pamoja na sehemu kubwa ya mapato ya mauzo ya nje, kwa mujibu wa takwimu za serikali. Tanzania ni mzalishaji wa nne kwa ukubwa wa dhahabu barani Afrika, ikitanguliwa na Afrika Kusini, Ghana na Mali, huku uzalishaji wa kila mwaka ukifikia wastani wa tani 50 hadi 60 katika miaka ya hivi karibuni.
Migodi mikubwa ya dhahabu inahusisha ile inayoendeshwa na kampuni ya Barrick Gold kwa ubia na Serikali ya Tanzania, pamoja na waendeshaji wengine wa kimataifa. Dhahabu inachangia sehemu kubwa ya mapato ya mauzo ya madini nje ya nchi, hali inayoifanya sekta hii kuathirika kwa kiwango kikubwa na mabadiliko ya bei katika soko la dunia.
Mbali na dhahabu, Tanzania ina akiba ya kibiashara ya almasi, makaa ya mawe na madini ya vito ya tanzanite, yanayopatikana kwa kiwango kikubwa zaidi katika Mkoa wa Manyara kaskazini mwa nchi. Aidha, Tanzania ina hifadhi kubwa ya madini ya nikeli, grafiti na madini adimu (rare earth elements), ambayo yanaonekana kuwa ya kimkakati kutokana na matumizi yake katika betri za magari ya umeme, hifadhi ya nishati jadidifu na viwanda vya teknolojia ya juu.
Mahitaji ya kimataifa ya grafiti na nikeli yameongezeka kwa kasi kufuatia jitihada za kupunguza hewa ukaa na kuhimiza matumizi ya umeme, jambo linalozifanya nchi za Afrika zenye rasilimali hizi kuwa kitovu cha mijadala ya minyororo ya ugavi duniani. Serikali ya Tanzania imesema inalenga kutumia fursa hii kuendeleza uwezo wa ndani wa uchakataji wa madini, badala ya kubaki msafirishaji wa malighafi.

Mageuzi ya sera na uongezaji thamani wa ndani
Katika miaka ya hivi karibuni, Tanzania imefanya mageuzi kadhaa ya kisera na kisheria ili kuimarisha ushiriki wa serikali, kuongeza uwazi na kurasimisha shughuli za wachimbaji wadogo na wa kati. Marekebisho ya sheria za madini yameweka mkazo katika maudhui ya ndani (local content), mifumo ya ugawaji mapato na uongezaji thamani wa madini.
Akizungumza katika mkutano huo mjini Cape Town, Waziri wa Madini, Antony Mavunde, alieleza mifumo ya kisheria na kikanuni inayosimamia sekta ya madini na kuainisha juhudi zinazofanywa kuongeza ushiriki wa Watanzania katika minyororo yote ya thamani ya madini.
Alisema mkakati wa serikali unaipa kipaumbele shughuli za uongezaji thamani ili kuongeza mapato yanayobaki nchini, kuunda ajira zenye ujuzi na kurahisisha uhamishaji wa teknolojia. Mkakati huo unajumuisha kuvutia uwekezaji katika mitambo ya kuyeyusha (smelting), kusafisha (refining) na kuchakata madini ndani ya Tanzania.
Majadiliano ya Indaba yalilenga ushirikiano katika uchakataji wa madini, utafiti wa kijiolojia na maendeleo ya madini muhimu. Wawekezaji pia walisisitiza umuhimu wa takwimu sahihi za kijiolojia ili kupunguza hatari za utafiti na kuongeza uhalali wa miradi kifedha.
Tanzania inatarajia kunufaika na mpango wa PanaAfGeo+ unaoungwa mkono na Umoja wa Ulaya, unaolenga kuimarisha uwezo wa utafiti wa kijiolojia barani Afrika kupitia mafunzo ya kitaalamu, msaada wa taasisi na uboreshaji wa mifumo ya usimamizi wa takwimu za kijiolojia.
“Ujenzi wa uwezo ulipewa msisitizo mkubwa, hususan katika mafunzo ya ufundi, matumizi ya teknolojia za kisasa na usimamizi wa takwimu za kijiolojia,” ilisema wizara hiyo.
Ujumbe wa Tanzania ulihusisha wawakilishi kutoka Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi (TISEZA), Chama cha Migodi Tanzania (TCM), Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Tanzania (FEMATA), Tanzania Youth in Mining (TYM) na Tanzania Women and Youths in Mining and Mineral Industry (TWiMMI), pamoja na kampuni za madini, taasisi za fedha na watoa huduma.
Maofisa walisema ushiriki huo unaonesha jitihada za serikali kuwaunganisha wachimbaji wadogo, vijana na wanawake katika minyororo rasmi ya thamani — hatua muhimu katika mkakati wa kupanua ushiriki wa kiuchumi katika sekta ya madini.
Kujipanga katika mazingira ya ushindani wa kikanda
Jitihada mpya za Tanzania kuvutia wawekezaji zinakuja wakati nchi za Afrika zikishindana kuongeza thamani ya rasilimali zao za madini, kufuatia mabadiliko ya minyororo ya ugavi duniani. Nchi kama Zambia na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo pia zinatafuta kupanua uchakataji wa shaba na kobalti ndani ya nchi, huku Afrika Kusini ikiendelea kuwa kivutio kikubwa cha uwekezaji wa madini.
Kwa kuhimiza uchakataji wa ndani, kuimarisha uwazi wa kisheria na kuwekeza katika takwimu za kijiolojia, serikali ya Tanzania imesema inalenga kuimarisha imani ya wawekezaji sambamba na malengo ya viwanda vya ndani.
Katika muktadha wa ongezeko la mahitaji ya madini yanayotumika katika nishati jadidifu na teknolojia za betri, maofisa wa serikali wanasema Tanzania inajiweka katika nafasi si tu kama mzalishaji thabiti wa dhahabu, bali pia kama msambazaji wa baadaye wa madini muhimu kwa masoko ya kimataifa — mradi miundombinu, ujuzi na mifumo ya ufadhili itaendelea kuboreshwa.
Serikali imeeleza dhamira yake ya kuongeza mchango wa sekta ya madini katika Pato la Taifa na mapato ya mauzo ya nje katika kipindi cha kati, huku ikihakikisha uzingatiaji wa mazingira, manufaa kwa jamii zinazozunguka migodi na uendelevu wa rasilimali kwa muda mrefu.








