DAR ES SALAAM/DODOMA: Mahakama ya Tanzania imesema imemaliza asilimia 93 ya kesi za kiuchumi na kibiashara zilizofanyiwa kazi kwa haraka katika kampeni ya wiki sita. Hatua hiyo ililenga kupunguza mrundikano wa kesi na kurejesha mabilioni ya shilingi kwenye mzunguko, hatua ambayo mamlaka inasema itaimarisha imani ya wawekezaji.
Msajili Mkuu, Eva Nkya, amesema kesi 2,973 zilisikilizwa kati ya Novemba 3 na Desemba 15, na kuvuka lengo la awali la kesi 2,128 zilizobainishwa wakati wa mkutano wa wadau mwezi Oktoba, huku kesi za ziada ziliingizwa baada ya nyingine kukamilika mapema kuliko ilivyotarajiwa, na kufanya jumla ya kesi zilizoshughulikiwa wakati wa vikao hivyo maalum kufikia 3,196.
Kesi hizo zilihusisha madai yenye thamani ya shilingi trilioni 13.1 ambayo ni sawa dola bilioni tano, fedha ambazo zilikuwa zimekwama katika mashauri ya kisheria kwenye ngazi mbalimbali za mfumo wa mahakama.
Mwanzoni mwa mpango huo, kesi 405 zilikuwa zinasubiri uamuzi katika Mahakama ya Rufani,
1,673 katika Mahakama Kuu, 17 katika Mahakama za Hakimu Mkazi na 33 katika Mahakama za
Wilaya. Kundi la awali la kesi 2,128 lilihusisha madai ya shilingi trilioni 4.4.
Tanzania yachukua hatua kali dhidi ya wakandarasi wasio waaminifu.
Nkya amesema zoezi hilo limepunguza mlundikano uliosalia katika kundi hilo hadi takriban asilimia
5 ya mzigo wa kesi, huku wastani wa muda wa kumaliza kesi ukishuka hadi siku 96. Mahakama za
mwanzo, ambazo hushughulikia zaidi ya asilimia 70 ya kesi nchi nzima, zilirekodi wastani wa
muda wa kumaliza kesi wa siku 30.
Vikao hivyo maalum viliratibiwa kwa ushirikiano na taasisi za umma na binafsi ikiwemo Ofisi ya
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Wizara ya Fedha, Benki Kuu, vyombo vya rufaa za kodi, vyama
vya mabenki na wafanyabiashara, na wanataaluma wa sheria.
Migogoro 18 ilitatuliwa kupitia upatanishi unaoongozwa na mahakama na mingine 25 ilitatuliwa
nje ya mahakama, ikiashiria msukumo wa kupanua mifumo mbadala ya utatuzi wa migogoro.
Kote Afrika Mashariki, mrundikano wa kesi za mahakamani na migogoro mirefu ya kibiashara
mara nyingi imekuwa ikitajwa na wawekezaji kama kikwazo cha kufanya biashara.
Mageuzi ya Tanzania yanakuja wakati serikali katika kanda hiyo zikitafuta kuboresha uhakika wa kisheria na kuharakisha ufufuo wa kiuchumi kufuatia mshtuko wa kimataifa ikiwemo janga la COVID-19 na
kuvurugika kwa mnyororo wa usambazaji.









