GENEVA: Rwanda imetoa wito wa kuundwa kwa mfumo wa kikanda wa kupambana na hotuba za chuki na kutokujali, ikionya kuwa uchochezi usiodhibitiwa, hasa kwenye mitandao, unatishia utulivu katika ukanda wa Maziwa Makuu.
Akizungumza jijini Geneva tarehe 23 Februari katika mapitio ya mfumo wa Umoja wa Mataifa dhidi ya ubaguzi wa rangi, Waziri wa Mambo ya Nje, Olivier Nduhungirehe, amesema lugha za uchochezi zinapohalalishwa au kutumiwa kisiasa, zinakuwa kichocheo cha vurugu.
Amesema itikadi ya kimbari iliyohusishwa na Mauaji ya Kimbari ya mwaka 1994 dhidi ya Watutsi imejipanga upya nje ya mipaka ya Rwanda, akiashiria kuendelea kuwepo kwa kundi la (FDLR) mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, ambalo ni kundi la waasi lililowekewa vikwazo na UN na lililoundwa na watu waliohusika na mauaji hayo.
“Hotuba za chuki huandaa mazingira,” amesema Alice Wairimu Nderitu, Mshauri Maalumu wa UN kuhusu Kuzuia Mauaji ya Kimbari, akibainisha kuwa mauaji ya 1994 yalitanguliwa na miaka mingi ya propaganda za kudhalilisha utu.
Waziri wa Sheria, Emmanuel Ugirashebuja, alisema Rwanda imefanya itikadi ya kimbari na ukanushaji kuwa kosa la jinai kama hatua ya kuzuia. “Lengo ni kusitisha vurugu kabla hazijaanza,” alisema








