BRUSSELS: Pesa ambazo Urusi ilipata kutokana na kuuza nje mafuta na gesi zimepungua katika kipindi cha miezi 12 iliyopita, hata wakati mauzo ya mafuta ya nchi hiyo yakiongezeka kwa kiasi, kulingana na takwimu zilizotolewa siku ya Jumanne, katika kumbukumbu ya miaka minne tangu uvamizi kamili wa Moscow dhidi ya Ukraine.
Urusi inategemea sana mapato ya nishati kusaidia vita vyake nchini Ukraine – uhusiano ambao umezifanya nchi za Magharibi kuweka vikwazo vikali zaidi kwa mafuta ya Urusi, zikijaribu kudhoofisha juhudi za kijeshi za nchi hiyo.
Uchambuzi uliochapishwa na shirika lisilo la kifaida la Kituo cha Utafiti wa Nishati na Hewa Safi (CREA) ulibaini kuwa mapato ya Urusi kutokana na mauzo ya nje ya mafuta, gesi, mkaa wa mawe na bidhaa zilizosafishwa yalifikia euro bilioni 193 katika kipindi cha miezi 12 kilichoishia Februari 24, 2026, ikiwa ni pungufu kwa 27% ikilinganishwa na kipindi kama hicho kabla ya uvamizi.
Wakati mauzo ya gesi ya Urusi yakiporomoka tangu 2022, vikwazo hadi sasa havijapunguza kiasi cha mauzo ya mafuta ya Urusi – badala yake, vimeilazimu Moscow kuuza mafuta kwa bei ya chini.
Mapato ya Urusi kutokana na mauzo ya mafuta ghafi katika miezi 12 iliyopita yalipungua kwa 18% kila mwaka, CREA ilisema. Wakati huo huo, kiasi cha mauzo ya mafuta ghafi kilisalia 6% juu ya viwango vya kabla ya uvamizi, kikiwa ni tani milioni 215.
Kujibu vikwazo vya Magharibi, Moscow imeelekeza sehemu kubwa ya mafuta yake yanayosafirishwa kwa njia ya bahari kwenda China, India na Uturuki, mara nyingi ikitegemea “msafara wa meli kivuli” (shadow fleet) wa meli za zamani, zisizo na bima ili kukwepa vikwazo vya Magharibi.
Lakini vikwazo vikali zaidi vinaweza kuathiri zaidi mauzo ya mafuta ya Urusi mwaka huu. Rais wa Marekani Donald Trump ameweka sharti la kuachana na mafuta ghafi ya Urusi ili kufikia makubaliano ya kibiashara na India.
Umoja wa Ulaya unajadili marufuku pana kwa biashara yoyote inayosaidia mauzo ya mafuta ghafi ya Urusi kwa njia ya bahari, hatua inayokwenda mbali zaidi ya vikwazo vya awali.
Umoja huo ulishindwa kupitisha vikwazo hivyo siku ya Jumatatu, baada ya Hungary kuweka kura ya turufu kutokana na mzozo kuhusu bomba la mafuta la Ukraine lililoharibiwa.
Urusi inasafirisha zaidi ya thuluthi moja ya mafuta yake kwa kutumia meli za nchi za Magharibi kwa msaada wa huduma za usafirishaji za Magharibi.
Marufuku hiyo inayopangwa na Umoja wa Ulaya itasitisha utaratibu huo, ambao kwa kiasi kikubwa unahudumia India na China, na kuifanya bei kikomo iliyowekwa na nchi za G7 kutoleta tija tena









