DODOMA, Tanzania: SPIKA wa Bunge, Mussa Zungu amesema kuna haja serikali ikaweka nguvu kwenye maeneo ya utalii wa kihistoria ya kidini na kutolea mfano wa msikiti wenye miaka zaidi ya 700 Kilwa mkoani Lindi.
Amesema kama Wizara ya Maliasili na Utalii ikijipanga vizuri kwa maeneo hayo inaweza kusaidia kupatikana kwa watalii zaidi ya milioni nne kwa mwaka kwa maeneo ya kihistoria ya kidini ikiwemo msikiti huo uliopo eneo la Songo Mnara, Kilwa, hivyo kuingiza fedha za kutosha.
Spika Zungu ametoa kauli hiyo leo Februari 6, 2026, muda mfupi baada ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Mipango na Uwekezaji), Prof Kitila Mkumbo kumaliza kufanya majumuisho ya hoja mbalimbali za wabunge kwenye hotuba yake kuhusu Mpango Elekezi wa Muda mrefu wa miaka 25 (2026/27 hadi 2050/51), Mpango wa Nne wa Maendeleo wa miaka mitano (2026/27 hadi 2030/31) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa wa mwaka 2026/27.
Amesema lazima mambo yaende kisasa, kwani Misri wanaingiza fedha kwa utalii kupitia maeneo ya kihistoa ya kidini, hivyo hata Tanzania hilo linawezekana kwa mipango imara ya maeneo ya kihistoria ya dini ya kiislamu na kikristo na kutolea mfano wa kanisa la Zanzibar lenye zaidi ya miaka 200.
Kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali Msikiti Mkuu wa Kilwa, unatajwa kwamba ni mkubwa zaidi kujengwa Kusini mwa Jangwa la Sahara katika karne ya 11.







