KOREA KUSINI: Mtanzania Gabriel Geay ametetea taji lake la mbio za Marathon za Daegu siku ya Jumapili,
akishinda katika hatua za mwisho za kusisimua na kujihakikishia ushindi wa mfululizo nchini
Korea Kusini.
Geay alivuka mstari wa kumalizia kwa kutumia saa 2, dakika 8 na sekunde 8, muda ambao ni sawa
na wa Muethiopia Chimdessa Gudeta, huku bingwa akipatikana tu kwa kumpita mwenzake kwa
kifu mbele kwenye utepe wa kumalizia.
Kasi hiyo ya mwisho ya Mtanzania huyo ilimpatia zawadi ya mshindi ya dola 200,000 na
kuthibitisha hadhi yake kama mmoja wa wakimbiaji bora wa marathon katika Afrika Mashariki.
Mbio hizo zilikuwa za kitalaamu zaidi kuliko mbio za kasi za kuvunja rekodi. Mtanzania mwenzake,
Emmanuel Dinday, aliweka kasi ya mapema akiongoza kundi katika kilomita 5 kwa kutumia dakika
15:05 huku wakimbiaji wakianza kutawanyika.
Katika hatua hiyo, Geay alikuwa akikimbia kwa tahadhari katika nafasi ya 14, akitunza nguvu huku
akibaki karibu na viongozi. Benard Geay alikuwa amejipanga nyuma yake kidogo.
Fikia kilomita 10, kundi la Watanzania lilikuwa limekaribia kundi la viongozi. Dinday alipanda
hadi nafasi ya tatu, Gabriel Geay nafasi ya nne, na Benard Geay akaingia kumi bora, ikionyesha nia
yao mbio zilipokaribia nusu ya safari.
Katika kilomita 15, Dinday aliongoza kwa dakika 44:22, huku Geay akiwa nyuma yake kwa
sekunde moja. Samson Hailemikael wa Eritrea na Gudeta walibaki karibu huku kundi la viongozi
likizidi kuwa dogo. Nusu ya safari (kilomita 21) ilifikiwa kwa dakika 58:43, huku wakimbiaji
wanne wakitofautiana kwa sekunde mbili pekee.
Hatua ya uamuzi ilianza baada ya kilomita 30. Gudeta alichukua uongozi kwa muda mfupi saa
1:28:12 huku kasi ikiongezeka, na Dinday aliyekuwa mstari wa mbele kwa sehemu kubwa ya mbio
alianza kuachwa na viongozi.
Geay alijibu mapigo katika kilomita 35, akichupa mbele kwa saa 1:43:55 na kuongeza kasi mpya.
Gudeta alienda naye hatua kwa hatua, na wawili hao walijitenga na kundi lingine kuelekea hatua za
mwisho.
Katika kilomita 40, Geay bado alikuwa na uongozi mwembamba wa saa 2:01:20, huku Gudeta
akimfuata kwa karibu. Dinday, ingawa hakuweza kuwafikia wawili hao, alipambana na kushika
nafasi ya tatu kwa saa 2:08:16, na kukamilisha matokeo mazuri kwa Tanzania. Benard Geay
alimaliza katika nafasi ya 13 kwa saa 2:15:45.
Mita za mwisho ndani ya Uwanja wa Daegu zilileta upinzani mkali. Wakikimbia bega kwa bega,
Geay na Gudeta waliongeza kasi ya ajabu. Katika mita za mwisho kabisa, Geay alipata nguvu ya
ziada na kuelekeza kifua chake mbele kwenye mstari ili kumshinda mpinzani wake kwa tofauti
ndogo mno.
Kwa kutwaa mataji mfululizo mjini Daegu, Geay amesisitiza kukua kwa nguvu ya Tanzania katika
mbio za masafa marefu na kuthibitisha uwezo wake wa kufanya vizuri chini ya shinikizo kubwa la
mashindano.








