ZANZIBAR: Magavana wa benki kuu kutoka kote kusini mwa jangwa la Sahara wametoa wito wa uratibu madhubuti wa kikanda ili kulinda utulivu wa kifedha wakati kutokuwa na uhakika wa kiuchumi duniani, kuongezeka kwa madeni, na mabadiliko ya haraka ya kiteknolojia vikibadilisha sura ya sekta ya fedha.
Wito huo umetolewa wakati wa mkutano wa Kikundi cha Mashauriano cha Kikanda cha Kusini mwa Jangwa la Sahara (RCG-SSA) cha Bodi ya Utulivu wa Kifedha (FSB), ulioandaliwa na Benki Kuu ya Tanzania (BoT) mjini Zanzibar.
Washiriki walijumuisha magavana na maafisa waandamizi kutoka benki kuu za Afrika Kusini, Zambia, Kenya, Ghana, Nigeria, Botswana, Angola, Uganda, Namibia, Mauritius, na Tanzania, pamoja na wawakilishi kutoka mamlaka za kifedha za kikanda za Afrika ya Kati na Magharibi.
Akifungua kikao hicho, Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Emmanuel Tutuba, amesema mivutano ya kijiopolitika, majanga yanayohusiana na hali ya hewa, kutokuwa na uhakika wa kisera, na athari za muda mrefu za janga la Uviko zimejaribu mifumo ya kifedha duniani kote.
“Mienendo hii imechochea shinikizo la mfumuko wa bei, kuongeza hatari za madeni, na kusababisha mabadiliko ya thamani ya sarafu, hali inayozibana serikali kifedha na kutatiza usimamizi wa uchumi mkuu,” amesema.
Mazungumzo hayo yamejikita katika uendelevu wa madeni, upatanishi wa kifedha usio wa kibenki, masoko ya mikopo binafsi, na hatari pamoja na fursa zinazohusiana na matumizi ya akili mnemba (AI) katika sekta ya fedha.
Gavana Lesetja Kganyago wa Benki ya Akiba ya Afrika Kusini (SARB) amesema kuwa nchi za kusini mwa jangwa la Sahara zinafanya kazi ndani ya mfumo wa kimataifa uliounganishwa, hivyo kufanya uratibu wa usimamizi kuwa muhimu katika kukabiliana na mishtuko inayovuka mipaka.
Gavana wa benki kuu ya Zambia, Denny Kalyalya, amesema jukwaa hilo linahakikisha kuwa mitazamo ya Afrika inaakisiwa katika utungaji wa sheria za kifedha duniani chini ya mfumo wa FSB.
FSB ilianzishwa na nchi za G20 mwaka 2009 kufuatia mgogoro wa kifedha duniani ili kuimarisha usimamizi wa mfumo wa kifedha wa kimataifa.
Mpango wake wa sasa wa kazi ni pamoja na kufuatilia hatari zinazohusiana na sarafu za kidijitali (stablecoins) na rasilimali nyingine za kidijitali, kuboresha maandalizi ya majanga, na kuendeleza mageuzi ya malipo yanayovuka mipaka.
Tutuba amesema uchumi wa Tanzania ulikua kwa wastani wa asilimia 6 kwa upande wa Bara na asilimia 6.8 kwa Zanzibar mwaka 2025, huku mfumuko wa bei ukibaki ndani ya lengo la asilimia 3– 5 kwa muda wa kati. Mikopo chechefu ilikuwa asilimia 2.8 mwishoni mwa Desemba, ikiwa chini ya kiwango cha ukomo cha asilimia 5, huku mikopo kwa sekta binafsi ikikua kwa asilimia 17.6.
Waundaji wa sera barani Afrika wamezidi kutafuta uwiano kati ya uvumbuzi wa kifedha na ujumuishi wa kifedha huku wakiweka kinga dhidi ya hatari za kimfumo, hususan wakati teknolojia ya kifedha (fintech) na matumizi ya pesa kwa njia ya simu yanapanuka kwa kasi barani kote









