DAR ES SALAAM — Kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani, Pope Leo, anatarajiwa kuanza ziara ya siku 10 barani Afrika Jumatatu, katika safari inayolenga kuelekeza macho ya dunia kwenye bara hilo lenye zaidi ya moja ya tano ya waumini wa Kanisa Katoliki duniani.
Ziara hiyo, ambayo ni miongoni mwa safari kubwa zaidi za kipapa katika miaka ya karibuni, itamfikisha katika nchi nne: Algeria, Cameroon, Angola na Equatorial Guinea. Kwa ujumla, atatembelea miji na maeneo 11, akisafiri takribani kilomita 18,000 kupitia safari 18 za ndege.
Afisa mwandamizi wa Vatican, Michael Czerny, alisema ziara hiyo inalenga “kuielekeza dunia kuitazama Afrika,” akisisitiza umuhimu unaoongezeka wa bara hilo ndani ya Kanisa Katoliki.
Akiwa na umri wa miaka 70, Papa huyo ambaye ni raia wa kwanza kutoka Marekani kushika wadhifa huo, anafanya moja ya safari ngumu zaidi kiupangaji tangu achaguliwe mwaka jana. Tangu wakati huo, amefanya ziara moja kubwa nje ya nchi pamoja na safari fupi katika mataifa mengine.
Afrika sasa inachangia zaidi ya asilimia 20 ya waumini wa Kanisa Katoliki duniani, huku nchi tatu kati ya atakazotembelea zikiwa na idadi kubwa ya waumini hao.
Hata hivyo, kituo chake cha kwanza kina mazingira tofauti. Algeria ina idadi kubwa ya Waislamu, ikiwa na chini ya waumini 10,000 wa Katoliki kati ya watu takribani milioni 48. Ziara hiyo itakuwa ya kwanza kwa nchi hiyo kumpokea papa aliyeko madarakani.
Kwa ujumla, hii itakuwa ziara ya 24 ya kipapa barani Afrika tangu miaka ya 1960, ikionyesha kuongezeka kwa umuhimu wa bara hilo katika Kanisa Katoliki duniani.
Msemaji wa Vatican, Matteo Bruni, alisema papa anatarajiwa kutoa hotuba 25 zitakazogusa masuala mbalimbali kulingana na hali za kila nchi. Mada kuu zinatarajiwa kujumuisha matumizi ya rasilimali za asili, mazungumzo kati ya dini tofauti, na hatari za rushwa ya kisiasa.
Mkusanyiko mkubwa zaidi unatarajiwa kufanyika nchini Cameroon, ambapo waumini wapatao 600,000 wanatarajiwa kushiriki ibada ya misa katika mji wa Douala.
Ziara hiyo pia inakuja katika mazingira ya kisiasa yenye tahadhari, ambapo baadhi ya nchi atakazotembelea zimekuwa zikikabiliwa na tuhuma za ukiukwaji wa haki za binadamu, ambazo zimekanushwa na serikali husika.
Papa Leo, anayezungumza lugha kadhaa, anatarajiwa kuzungumza na waumini na viongozi kwa lugha mbalimbali kulingana na mazingira ya kila nchi.
Atakapoanza ziara yake nchini Algeria, atakutana na viongozi wa kisiasa kabla ya kutembelea msikiti mkubwa wa Algiers, ikiwa ni mara ya pili kwa yeye kutembelea msikiti tangu achaguliwe. Baadaye atasafiri hadi Annaba kutembelea magofu ya kale ya Hippo, eneo lenye umuhimu wa kihistoria katika Ukristo.








