N’DJAMENA: Chad imefunga mpaka wake wa mashariki na Sudan siku ya Jumatatu baada ya mapigano ya wikendi yanayohusiana na vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Sudan kuua wanajeshi watano wa Chad, vyanzo viwili viliiambia Reuters.
Mzozo nchini Sudan kati ya jeshi la Sudan na kikosi cha wanajeshi wa akiba (Rapid Support Forces – RSF), uliopuka Aprili 2023, umekuwa ukivuka mara kwa mara kuingia katika ardhi ya Chad, na kusababisha vifo na uharibifu wa mali.
Afisa wa Chad aliiambia Reuters kuwa mapigano ya Jumamosi kati ya RSF na wapiganaji wa kundi la wanamgambo wanaounga mkono serikali ya Sudan katika mji wa mpakani wa Tine yaliua wanajeshi watano na raia watatu, na kujeruhi watu 12.
Afisa wa walinda mpaka mjini Tine alithibitisha vifo vya wanajeshi hao watano na kusema kuwa hatua za ziada za usalama zinahitajika ili kulinda raia upande wa Chad.
Vyanzo viwili, vilivyozungumza kwa sharti la kutotajwa majina kwa sababu havikuwa na idhini ya kuzungumza na vyombo vya habari, vilisema wanajeshi zaidi wa Chad walikuwa wakipelekwa katika eneo hilo.
Serikali ya Chad ilisema siku ya Jumatatu kuwa mpaka huo utabaki kufungwa hadi itakapotangazwa tena, ikitaja “uvamizi na ukiukwaji wa mara kwa mara unaofanywa na vikosi katika mzozo wa Sudan.”
Hatua hiyo “inalenga kuzuia hatari yoyote ya mzozo huo kusambaa kwenye ardhi yetu, kulinda wananchi wetu na wakimbizi, na kuhakikisha utulivu na mamlaka ya nchi yetu,” taarifa ya serikali ilisema.
Jeshi la Sudan na RSF hawakujibu mara moja maombi ya kutoa maoni. Mwaka jana, shambulio la ndege isiyo na rubani (drone) liliua wanajeshi wawili wa Chad, kulingana na mamlaka za mitaa na chanzo cha usalama, ingawa haikuwa wazi ni nani aliyefanya shambulio hilo.
“Jambo moja ni hakika: tupende au tusipende, Chad sasa inaonekana kuwa upande katika mzozo huu,” alisema Ahmat Yacoub kutoka Kituo cha Mafunzo ya Maendeleo na Kuzuia Itikadi Kali.








